Makalla ajitosa sakata la Jaydee, Clouds
NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Amos Makalla
amejitokeza kusuluhisha mgogoro kati ya Kampuni ya Clouds na msanii Judith
Wambura ‘Lady Jaydee’.
Clouds na Jaydee wamejikuta katika mgogoro siku za karibuni,
unaohusishwa na madai ya msanii huyo kuminywa kazi zake kuchezwa katika vituo
vya redio na televisheni, mali ya kampuni hiyo ya utangazaji.
Lakini jana katika taarifa yake hapa, Makalla alisema yupo tayari
kukutana na pande hizo mbili kusaka suluhu la kudumu la mgogoro huo, akisema
malumbano hayana tija na yanakuza mgogoro.
“Kutokana na malumbano ya Jide (jina jingine la Jaydee) na uongozi
wa Clouds, natoa mwito nikutane na pande mbili. Nawasihi sana malumbano hata
hayatakuwa na tija, bali kukuza mgogoro uliopo sasa,” alisema Naibu Waziri
Makalla.
Alisema yupo tayari kukutana na pande zote mbili, uongozi wa
Clouds na Jaydee na meneja wake, Gadner Habash ambaye pia ni mumewe, wakae na
kujadili mambo hayo.
“Sifurahi hata kidogo jambo hili linaloendelea halijengi. Nimsihi
sana mdogo wangu na shemeji yangu Jide, akubali tukae pamoja na niwaombe Clouds
wakubali tukae pamoja. Naamini tukikaa pamoja tutaongea jambo hili litakwisha,”
alisema Makalla.
Katika mzozo huo, Jaydee anayemiliki Bendi ya Machozi na Mgahawa
wa Nyumbani Lounge, anawalaumu Mkurugenzi wa Utafiti wa Clouds, Ruge Mutahaba,
na mmiliki wa kampuni, Joseph Kusaga, kuwa wanamzibia kupata riziki katika kazi
zake.
Jaydee ambaye amekuwa akitoa shutuma hizo kupitia blogu yake na
mitandao ya kijamii, alienda mbali zaidi na kueleza kuwa ikitokea amekufa,
hataki kituo hicho kiomboleze kifo chake wala hataki wakurugenzi hao waende
katika msiba wake.
Akizungumzia tuhuma hizo Mkurugenzi wa Utafiti wa Cloud Fm
Rugemalila Mutahaba aliliambai gazeti hili kituo hicho kipo tayari muda wowote
na saa yoyote kulitafutia ufumbuzi suala hilo.
Alisema kuwa kwanza bado hadi sasa hawajajua sababu kubwa hasa za
msanii huyo kuwakasirikia na hata hivyo wapo tayari kukutana na sio Jide peke
yake ila mtu yoyote mwenye malalamiko kuhusiana na kituo hicho.
" Najua sisi ni wanadamu na huenda kuna mambo ambayo
tunayafanya katika kutimiza wajibu wetu lakini tukawa kwenye mzozo nawatu
wengine sasa basi kwanza tunamshukuru Naibu Waziri kwa juhudi zake hizo na sisi
saa yoyote tupo tayari kukutana kulijadili suala hilo" alisema Rugemalila.
Kwa upande wake Meneja wa Lady Jaydee, Gadner Habashi hakupatikana
kuzungumzia suala hilo ambapo simu yake ilikuwa ikiita bila ya kujibiwa.
Mwisho
0 comments: